Add parallel Print Page Options

Simulizi Kuhusu Mkulima Aliyepanda Mbegu

(Mk 4:1-9; Lk 8:4-8)

13 Siku hiyo hiyo Yesu alitoka nje ya nyumba na kukaa kando ya ziwa. Kundi kubwa wakakusanyika kumzunguka. Hivyo akapanda mtumbwini na kuketi. Watu wote wakabaki ufukweni. Kisha Yesu akatumia simulizi kuwafundisha mambo mengi. Akawaambia simulizi hii:

“Mkulima alitoka kwenda kupanda mbegu. Alipokuwa anatawanya mbegu, baadhi ziliangukia njiani. Ndege wakaja na kuzila zote. Mbegu zingine ziliangukia kwenye ardhi yenye mawe, ambako hakukuwa na udongo wa kutosha. Zikakua haraka pale, kwa sababu udongo haukuwa na kina. Lakini jua lilipowaka, likaichoma mimea. Mimea ikafa kwa sababu haikuwa na mizizi mirefu. Baadhi ya mbegu ziliangukia katikati ya miiba. Miiba ikakua na kusababisha mimea mizuri kuacha kukua. Lakini baadhi ya mbegu ziliangukia kwenye udongo wenye rutuba. Hapo zikakua na kuzaa nafaka. Baadhi ya mimea ikazaa nafaka mara mia zaidi, baadhi mara sitini na baadhi mara thelathini zaidi. Ninyi watu mnaoweza kunisikia, nisikilizeni!”

Kwa nini Yesu Alitumia Simulizi Kufundisha

(Mk 4:10-12; Lk 8:9-10)

10 Wafuasi wake wakamwendea Yesu na kumuuliza, “Kwa nini unatumia simulizi hizi kuwafundisha watu?”

11 Yesu akawajibu, “Mungu amewapa ninyi ujuzi wa kuelewa siri za ufalme wa Mungu, lakini hajawapa watu hawa wengine ujuzi huu. 12 Kisha akawaambia, ‘Zingatieni kwa makini kile mnachokisikia. Kwani jinsi mnavyosikiliza kwa makini, ndivyo mtakavyoelewa na kuzidi kuelewa. Kwa kuwa kila aliye na uelewa kidogo ataongezewa zaidi. Lakini wale wasiosikiliza kwa makini watapoteza hata ule uelewa mdogo walio nao.’ 13 Ndiyo sababu ninatumia simulizi hizi kuwafundisha watu: Wanaona, lakini hakika hawaoni. Wanasikia, lakini hakika hawasikii au kuelewa. 14 Hiyo inathibitisha alichosema nabii Isaya kuhusu wao kuwa kweli:

‘Ninyi watu mtasikia na kusikia,
    lakini hamtaelewa.
Mtatazama na kutazama,
    lakini hakika hamtaona.
15 Ndiyo, akili za watu hawa sasa zimefungwa.
    Wana masikio, lakini hawasikii vizuri.
Wana macho, lakini wameyafumba.
    Iwapo akili zao zisingekuwa zimefungwa,
wangeona kwa macho yao;
    wangesikia kwa masikio yao;
Iwapo wangeelewa kwa akili zao.
    Kisha wangenigeukia na kuponywa.’(A)

16 Bahati gani mliyonayo ninyi. Mnaelewa mnachokiona kwa macho yenu. Na mnaelewa mnachosikia kwa masikio yenu. 17 Ninaweza kuwathibitishia, manabii na watakatifu wengi walitaka kuona mnayoyaona. Lakini hawakuyaona. Walitaka kusikia mnayosikia sasa. Lakini hawakuyasikia.

Read full chapter